Saturday, July 31, 2010
   
Text Size

Tafuta kwenye Website hii

Mramba aibuka kwa mapadri, masheikh

Mbunge wa Rombo, Basil Mramba (CCM), amekutana na viongozi wa dini za Kikristo na Kiislamu pamoja na wa serikali kuzungumzia maendeleo ya wilaya na kutumia fursa hiyo kuwaomba viongozi hao wamuunge mkono nia yake ya kutetea kiti cha jimboni hilo, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.

Katika mkutano huo uliofanyika Machi 2, mwaka huu katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Peter Toima, na kuhudhuriwa na mapadri wa Kanisa Katoliki na masheikh wa wilaya hiyo, Mramba aliwaeleza kuwa ana nia ya kuwania ubunge katika jimbo hilo mwaka huu.

Taarifa kutoka katika mkutano huo, uliochukua zaidi ya saa tano, zinadai kuwa Mramba alichelewa kufika na kukuta mkutano ukiendelea na katika mazungumzo yake, aliwaomba viongozi hao kufikisha salamu kwa waumini wao na kuhakikisha wanamuunga mkono ili aweze kufanikiwa.

Aidha, aliwaomba viongozi hao kumsaidia ili aweze kurejea tena katika nafasi hiyo na kuwaeleza wazi kuwa bado ana nia ya kuwania ubunge katika jimbo hilo na kwamba nia yake itakwama tu kama Chama Cha Mapinduzi (CCM) hakitampa ridhaa.

Wakizungumzia ombi hilo, ambalo ni nadra sana kutokea, hasa katika kipindi hiki, ambacho joto la uchaguzi limepanda katika maeneo mbalimbali nchini, baadhi ya viongozi walidai wana taratibu zao za kufanya kazi na hawawezi kuburuzwa na wanasiasa.

Sisi kama viongozi wa dini tuna taratibu zetu za kufanya kazi, kama mtu ametuita na ameonyesha nia ya kuwania ubunge,” alisema kiongozi mmoja wa dini na kuongeza: “Sisi tunamsikiliza na kuwaachia maamuzi wapigakura, ambao ni wananchi kwani hatuwezi kuwaambia wamchague nani na kumuacha nani.”

Alisema kwa sasa nchi ikiwa inaelekea katika uchaguzi mkuu Oktoba mwaka huu, wanajitokeza watu wengi na kuongea nao, lakini wao wanawasikiliza wananchi pekee ndiyo wenye maamuzi.

Akizungumzia mkutano huo ambao ulihudhuriwa pia na Katibu Tawala wa wilaya hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo na viongozi wengine wa serikali, Mkuu wa wilaya hiyo alisema mkutano huo aliuitisha yeye kwa lengo la kukutana na viongozi hao wa dini kujadilia masuala ya maendeleo ya wilaya hiyo.

Alisema kuwa hakujua Mramba alitokea wapi na kuhudhuria mkutano huo na kwamba hakumwalika, lakini kwa kuwa alifika alipewa nafasi ya kuzungumza na viongozi hao kama mbunge wao.

Sikumuita Mbunge (Mramba), yeye alihudhuria kama mtu mwingine ambaye angeruhusiwa kuhudhuria, kama ungekuwa mkutano wa viongozi wa siasa lazima ningemuita Mwenyekiti wa CCM mkoa na Katibu,” alisema DC Toima na kuongeza: “Mkutano wangu ulikuwa wa kawaida na si wa kisiasa.”

Toima alisema mkutano huo ulijadili ushirikishwaji wa viongozi wa dini katika masuala ya maendeleo ya afya, maji, miundombinu na masuala mengine ya maendeleo ya wilaya hiyo.

Alipohojiwa juu ya hatua ya kuitisha mkutano huo wakati kukiwa na joto la uchaguzi, alisema yeye si kiongozi wa siasa bali ni mtumishi wa serikali na kwamba hachanganyi siasa na dini na endapo kiongozi mwingine wa siasa angefika katika mkutano huo angeruhusiwa kuhudhuria.

Siku hiyo hiyo, majira ya saa 7 mchana, Mramba alizungumza na wachungaji wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini katika mkutano ulioitishwa na Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Aloyce Kimaro (CCM).

Mkutano huo ulifanyika makao makuu ya jimbo la Kilimanjaro Mashariki, katika mji mdogo wa Himo chini ya uenyekiti wa Mkuu wa Jimbo hilo, Luca Kessy.

Katika mkutano huo, Mramba alisema licha ya kukabiliwa na kesi mahakamani, bado ataendelea kuwa mbunge wa jimbo hilo kwani wananchi wake bado wanampenda na watampa nafasi tena ya kuwawakilisha bungeni.

Alisema ni mzoefu wa kesi na kwamba ana uzoefu katika utendaji kazi serikalini na ubunge kwani amekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa vipindi vitatu tofauti.

Aligusia kesi ya jinai inayomkabili mahakamani kuwa inamnyima nafasi ya kuwahudumia vyema wananchi wake.

Mramba alisema si kila mwanaume anayevaa suruali au mwanamke anayevaa sketi anastahili kuwa mbunge, hivyo ni vyema wananchi wakawa makini sana na watu wanaojipitisha pitisha katika majimbo yao.

Siasa siyo kamari, kuwa kiongozi ni lazima uwe na wito fulani ndani yako na vile vile siasa ni kazi mbaya,” alisema bila kufafanua.

Aidha, aliwabeza baadhi ya wabunge, ambao kwa sasa wanahaha katika majimbo yao kwa kurudi kuwabembeleza wananchi dakika za mwisho ilhali muda wao wa miaka minne waliutumia kwa kukaa jijini Dar es Salaam na kuishi maisha ya starehe.

Dunia ina watu wazuri na wabaya, tunaishi nao na tunafanyakazi nao, mimi ni mzoefu wa kushtakiwa na hilo halinikatishi tamaa ya kuwatumikia wananchi wangu ambao bado wana imani kubwa na mimi,” alisema.

Hivi karibuni, Katibu wa CCM mkoani hapa, Steven Kazidi, alikaririwa akiwataka viongozi wa dini kutokubali makanisa kutumika kama majukwaa ya kisiasa hasa katika kipindi hiki cha kuelekea katika uchaguzi huo.

 

CHANZO: NIPASHE
Comments
Add New Search
Write comment
Name:
Email:
 
Title:
UBBCode:
[b] [i] [u] [url] [quote] [code] [img] 
 
 
Please input the anti-spam code that you can read in the image.

3.26 Copyright (C) 2008 Compojoom.com / Copyright (C) 2007 Alain Georgette / Copyright (C) 2006 Frantisek Hliva. All rights reserved."

Habari Motomoto

  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
  • 6
  • 7
  • 8
  • 9
  • 10
  • 11
  • 12
  • 13
  • 14
  • 15
  • 16
  • 17
  • 18
  • 19
  • 20

Login Form